Monday, July 28, 2014

CHEKI HII; MAAJABU YA MCHEZO WA SOKA WA KENGELE KWA VIPOFU

 
“Kabla ya kuanza mechi, kocha unatakiwa kumchukua mchezaji mmoja mmoja na kumzungusha eneo zima la uwanja kwa dakika 30, tunafanya hivyo ili kumjengea mchezaji hali ya kuzoea mazingira ya uwanja kabla ya kucheza,” anasema kocha wa mpira wa kengele, Hashiru Tembo
Anasema wachezaji hupelekwa kila sehemu ya uwanja utakaotumika kwenye mechi hiyo, ambazo ni kwenye goli wanalotakiwa kufunga na kwenye goli lao kwa ajili ya kuzuia na mwisho wa uwanja, pia katikati ili kung’amua urefu na ukubwa wa uwanja watakaoutumia.
Mpira wa kengele au ‘Goal ball’ ni mchezo ulioanzishwa na raia wa Australia, Hanzi Lorenzen na raia wa Ujerumani, Sepp Reindle mwaka 1946 kwa ajili ya kuwasaidia askari waliopigana vita ya pili ya dunia na kupata matatizo ya macho.
Kwa mara ya kwanza nchini mchezo huu umechezwa kwenye mashindano ya 20 ya Umoja wa Michezo na Taaluma kwa Shule za Msingi Tanzania (Umitashumta) ya msimu huu kwenye viwanja vya Shirika la Elimu Kibaha, Pwani.
 
Mpira wa kengele unavyochezwa
Hashiru Tembo ambaye ni kocha wa mchezo huo anasema mpira wa kengele unachezwa na wachezaji wasioona (vipofu) na wenye uoni hafifu ambao kabla ya kuanza kwa mechi wote huvaa vitambaa vyeusi kuziba macho kwa ajili ya kuzuia wale wenye uoni hafifu kutoona kabisa ili kuendana na wenzao (vipofu).
Timu nzima ina wachezaji wangapi?
Tembo anasema kila timu inasajili wachezaji wanne, ambao kati yao watatu wanakuwa kwenye kikosi cha kwanza na mmoja anakuwa mchezaji wa akiba, wanaoanza mmoja anakuwa mchezaji wa kati na wachezaji wawili wa pembeni.
“Mchezaji wa kati mara nyingi anakuwa yule mwenye hisia za haraka za kubaini mpira pale unapokuwa umerushwa golini kwao na anapoudaka hatakiwi kuugusa zaidi ya mara mbili, akishagusa mara mbili anapaswa kumpa mchezaji wa pembeni akigusa mara ya tatu hiyo ni faulo,” anasema Tembo.
Anasema mchezaji wa kati ambaye ni muhimu kwa ulinzi anapougusa mpira kwa kuwa ni mchezo wa wasioona, anapaswa kufanya ishara ya kugusa mpira kwa nguvu kidogo ili kengele itoe sauti kumwashiria yule wa pembeni kuwa anampa pasi.
“Akiugusa mara ya tatu hiyo ni faulo, na faulo za mpira wa kengele ni kupigwa kwa penati, wakati wa upigaji wa penati wachezaji wa pembeni wanapaswa kutolewa na kubaki yule wa kati peke yake,” anasema Tembo.
 
Anasema mpira wa kengele hauna kona wala mpira wa kurusha, goli linapofungwa timu iliyofungwa ndiyo inaanzisha mpira kutoka pembeni mwa goli lao na mchezaji atakayetoa nje mpira unapelekwa kuanzwa kwenye lango la timu pinzani.

No comments:

Post a Comment