Sunday, July 27, 2014

SAKATA LA KUOKOTWA VIUNGO VYA BINADAM; MUHAS YASEMA: Tunatumia maiti 25 kwa mwaka kufundishia


Wakati sakata la kuokotwa kwa viungo vya binadamu likiendelea kutikisa nchi, Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS), kimesema kuwa hutumia maiti 25 kwa kuwafundishia wanafunzi kila mwaka.

Pia chuo hicho hakijawahi kuagiza maiti kutoka nje ya nchi na kwamba ni mtu mmoja tu aliyewahi kutaka maiti ya mtoto wake itumike kufundishia.
Kauli hiyo ya MUHAS imekuja siku chache baada ya Serikali kuamua kuifungia Hospitali ya Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Tiba na Teknolojia (IMTU), baada ya kubaini kasoro kadhaa katika utendaji wake.
Juzi, Serikali ilifanya ukaguzi wa kushtukiza IMTU, baada ya hospitali hiyo kukumbwa na kashfa ya utupaji wa mabaki ya viungo vya binadamu katika Bonde la Mto Mpiji, jijini Dar es Salaam mwanzoni mwa wiki iliyopita.
Hata hivyo, wakati Tume ya Watu 15 iliyoundwa na Serikali kuchunguza suala hilo ikiendelea na kazi, Mkuu wa Kitengo cha Anatomy MUHAS, Profesa David Ngassapa amebainisha kuwa chuo hicho hutumia maiti 25 kwa mwaka.
Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake jana, Ngassapa alisema kuwa wanafunzi wa mwaka wa kwanza hutumia maiti 20, huku madaktari wanaorudi chuoni hapo kwa ajili ya mazoezi wakitumia maiti tano.

No comments:

Post a Comment